Events
MKURABITA kushiriki kikao cha mashauriano cha wadau wa urasimishaji wa biashara ndogo na watoa huduma kwa wamachinga

Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA)
kwa kushirikiana na Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeandaa kikao cha mashauriano
cha wadau wa urasimishaji biashara kitakachofanyika tarehe 6 Oktoba 2022 katika
eneo la Soko la Machinga Barabara ya Bahi, Dodoma kuanzia saa saa 03.00 asubuhi.
Mratibu wa Mpango CPA. Dkt. Seraphia Mgembe anatarajia kufungua kikao hicho
kitakacho hudhuriwa na wadau kutoka taasisi zipatazo 20 ambazo ni pamoja na Wizara
ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Wizara ya Uwekezaji,
Viwanda na Biashara, Ofisi ya Rais TAMISEMI, NIDA, TRA, NSSF, Ofisi ya Katibu
Tawala wa Mkoa, Ofisi ya Kamanda wa Polisi Wilaya –OCD, Umoja wa Wamachinga –
Dodoma. Kikao hiki pia kitahudhuriwa na wawakilishi kutoka taasisi za fedha ikiwemo
CRDB Bank, NMB Bank, NBC, Equity Bank na Amana Bank.
Aidha, kikao kimeandaliwa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya utekelezaji wa Agizo
lililotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Samia Suluhu Hassan
la kuzitaka Mamlaka zote nchini kuwapanga wamachinga ili kuwawezesha kufanya
biashara zao kwa tija katika miji mbalimbali nchini. Mheshimiwa Rais, aligiza Wakuu wa
Mikoa nchini kuhakikisha kuwa wafanyabiashara wa kundi la machinga wanapangwa ili
waweze kufanya biashara katika mazingira yenye miundombinu wezeshi itakayotoa
fursa za kukuza biashara zao. Pia aliwataka akuu wa Mikoa, Wilaya na Wakurugenzi
wa Halmashauri kushirikiana katika kujenga na kusimamia masoko ya
wafanyabiashara (Machinga) katika maeneo yao.
Sambamba na ujenzi wa miundombinu wezeshi kwa wafanya biashara wadogo
Mheshimiwa Rais pia alielekeza kuandaliwa kwa mafunzo maalum kwa ajili ya
Machinga ili kuwawezesha kuwa na sifa za kukopesha kwenye Taasisi za fedha kwa
masharti nafuu, kuwepo na dawati la kushughulikia Sera na Miongozi ya machinga,
kuboreshwa kwa vitambulisho vya machinga ambavyo vitabainisha shughuli
wanazozifanya, sehemu ya biashara, aina ya biashara na sehemu anapoishi.
Katika kufanikisha azma yake na kutekeleza maagizo ya Mheshimiwa Rais na uzoefu
wa MKURABITA katika kuyafikia makundi maalum, tayari imeanzisha mradi wa
urasimishaji na uendelezaji biashara za makundi hayo ikiwemo machinga na
waendesha bajaji na bodaboda.